Jumatatu , 24th Oct , 2022

Jeshi la polisi Nchini limetoa ufafanuzi kuhusu tukio la mauaji yaliyotokea Oktoba 23 mwaka huu katika kijiji cha Ikwambi Wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro yaliyotokea wakati Jeshi la polisi likiziua uvunjifu wa amani kati ya wakulima na wafugaji.

IJP Camillus Wambura

Akitoa ufafanuzi huo Mkuu wa jeshi la polisi nchini IJP Camillus Wambura amefafanua kuwa wakuliwa walikuwa na malalamiko ya jamii ya wafugaji kulisha mifugo yao kwenye mazao yao huku pia wakidai kuwa wakulima wenzao wawili walishambuliwa wafugaji Oktoba 22, 2022.

 

Kutokana na malalamiko hayo jamii ya wakulima waliamua kujichukulia sheria mkononi kwa kuwakamata viongozi wa kijiji hicho na pamoja na Mkaguzi wa kata na kuwafungia kwenye ofisi ya kijiji na Oktoba 23, Polisi walipofika katika eneo hilo ka lengo la kuwaokoa viongozi hao ndipo ikatokea tafrani iliyopelekea matumizi ya risasi za moto na mabomu ya machozi yaliyosababisha vifo vya watu hao wawili.

 

Aidha IJP Wambura amebainisha kuwa timu maalamu imeundwa chini ya uongozi wa wa Mkurugenzi wa Mashtaka pamoja na taasisi nyingine za serikali kwa madhumuni  ya kufanya uchunguzi huru utakaowezesha kupata majibu ya chanzo cha tukio hilo.

 

Jeshi la Polisi limewataka wananchi wa Kijiji cha Ikwambi kuwa watulivu katika kipindi hiki huku pia askari waliohusika katika tukioa hilo, wakikaa kando kupisha uchunguzi wa tukio hilo na kuliagiza Jeshi la Polisi Wilaya ya Kilombero kutoa ushirikiano kwa timu iliyoundwa kufanya uchunguzi.