Jumatano , 5th Apr , 2023

Hatimae Mahakama ya Hakimu mkazi Moshi imemuachia huru aliyekuwa Mkuu wa wilaya ya hai Mkoani Kilimanjaro Lengai Ole Sabaya ambaye alisalia peke yake katika kesi ya uhujumu uchumi namba 2,2022

Awali katika kesi hiyo Sabaya alikuwa na wenzake wanne ambao ni Sylvester Nyegu, Nathan Msuya, John Aweyo na Antero Asey ambao  Septemba 7.2022 waliachiwa huru kwa makubaliano nje ya Mahakama na Mwendesha mashtaka Mkuu wa serikali.

Msingi wa kesi hiyo kwa Mujibu ya hati ya mashtaka inadaiwa Mnamo Februari 21.2021 Sabaya na waliokuwa wenzake hao walijipatia kitita cha shilingi milioni 50 kutoka kwa mfanyabiashara Alex Swai Wakimtisha kutoa taarifa zake za ukwepaji kodi.

Ikumbukwe pia tangu kesi hiyo kuanza kwake Juni 1.2022 haikuwahi kusikilizwa kutokana na sababu mbalimbali za kisheria.

Kesi hiyo inayosikilizwa na Hakimu Mkazi Salome Mshasha leo Aprili 05.2023 ilifika Mahakamani kwa ajili ya kutajwa lakini upande wa mashtaka kupitia kwa wakili mwandamizi wa serikali Verediana Mlenza akadai mshtakiwa ameomba makubaliano nje ya Mahakama na Mwendesha mashtaka Mkuu wa serikali.

Maombi ambayo Mahakama iliyaridhia na kumuachia huru Mshtakiwa huyo Lengai ole Sabaya kwa sharti la kifungo cha nje kwa muda wa mwaka mmoja, na kumtaka amlipe  fidia ya shilingi milioni 5 mfanyabiashara Elbariki Swai ambaye ni Muathirika wa tukio hilo