Ijumaa , 16th Nov , 2018

Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema amekiri kuwa na mahudhurio hafifu ndani ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kile alichokisema kuwa ni kukabiliwa na majukumu mengine ya nje ya ubunge, ambapo aliitaja sababu ya kuhudhuria kesi mbalimbali mahakamani.

Mbunge wa Arusha Mjini Godbless Lema, Spika wa Bunge Job Ndugai/.

Kauli hiyo ya Lema imekuja siku moja baada ya Spika Job Ndugai kumtaja mbunge huyo pamoja na Mbunge wa Kibamba John Mnyika wako kwenye orodha ya wabunge ambao wana mahudhurio hafifu kwenye bunge la hilo.

Akizungumza na www.eatv.tv Lema amesema “sisi ni wabunge ambao tuna kesi nyingi mahakamani, kwenye bunge la bajeti nilihudhuria mahakamani mara 4 kwa mwezi, kwa misingi kama hiyo lazima utakuwa na mahudhurio hafifu bungeni.”

Mimi pia nimekaa jela miezi 5 na spika amesahau kule jela hakuna bunge, na nilikamatwa wakati wa bunge na nikaachiwa kipindi ambacho bunge limeisha,” ameongeza Lema

Kingine huwezi kuhudhuria bungeni kila siku, ni lazima uwe na hoja mimi mahudhurio yangu huwa yanamchango sana kwa taifa hasa kwenye uchumi, siasa na haki za binadamu lakini wao wanawabunge wengi ambao wanahudhuria bungeni kama wanafunzi wa darasa la kwanza,” ameongeza Lema.

Aidha Lema amesema “Lakini mimi ni mwakilishi wa jimbo kuna wakati naenda kufanya kazi jimboni au kuwatafutia misaada wananchi wangu, pia mbunge ni mwakilishi wa chama mimi kwangu nimefanya uchaguzi mara mbili kwa hiyo nisingeweza kuhudhuria bunge".

Yapo mengi sana lakini bado uwepo wetu kila tunapopata nafasi ya kuingia bungeni huwa tunatoa michango ambayo ni muhimu sana kwa taiifa,” amemalizia Lema.