Alhamisi , 25th Jun , 2015

Serikali imeshauriwa kuzuia matumizi mabovu ya fedha za umma pamoja na kuziba mianya ya rushwa inayopelekea serikali kushindwa kukusanya mapato yake na kutafuta njia mbadala ambazo zinaonekana kuwaumiza wananchi.

Mbunge wa Kigoma kusini Mh, David Kafulila.

Akichangia muswada wa sheria ya fedha uliowasilishwa leo bunge na waziri wa fedha, mbunge wa Kigoma kusini Mh, David Kafulila amesema kuwa serikali imekuwa na matumizi mabovu na yanovunja sheria yanayopeleka nchi kukosa mapato.

Mh. Kafulila ametaka serikali kutoa ripoti ya upotevu wa takribani bilioni 238 ambazo zilitumika kununuliwa mabehewa ambayo hayakidhi viwango na kuongeza serikali imekosa ubavu wa kuvikabili vyanzo vikubwa vya ukusanyaji wa mapato.

Mbunge huyo amesema kuwa endapo fedha hizo zingepatikana kusingekuwa na haja ya kuongeza tozo ya mafuta ka ajili ya shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo ya kusambaza umeme vijijni na Maji kama bajeti ya mwaka huu ilivyotoa kipaumbele.

Aidha ameongeza kuwa Tanzania imekuwa kinara wa Uingizaji wa Bidhaa feki ambazo zinaingia katika bandarini na mamlaka husika kushindwa kuchukuwa hatua madhubuti za kudhibiti suala na kufanya serikali kupoteza imani na wananchi.

Amesema kuwa ulipaji wa kodi ni imani ambayo wananchi wanayo juu ya serikali yao lakini kutokana na wananchi wa Tanzania kukosa imani ndiyo kunawafanya wafanyabaishara wengi kutokuona umuhimu wa ukusanyaji wa kodi hizo.