Alhamisi , 3rd Nov , 2016

Serikali imesema inaendelea kuboresha na kuongeza vituo vya kuhudumia watoto wanaozaliwa kabla ya wakati na wenye uzito mdogo katika kila wilaya ili kupunguza vifo vya watoto wachanga nchini.

Dkt. Hamis Kigwangalla, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

 

Akiongea Bungeni Mjini Dodoma hii leo katika Kipindi cha Maswali na Majibu Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangalla, amesema kuwa asilimia 25 ya vifo vya watoto hao vinatokana na watoto wanaozaliwa kabla ya wakati na wenye uzito mdogo.

Dkt. Kigwangalla ameongeza kuwa serikali ilianzisha huduma ya matunzo ya mtoto aliyezaliwa kabla ya wakati kwa kumbeba mtoto ngozi kwa ngozi (Kangaroo method), ili kuweza kuwa katika uhalisia na mazingira bora kutoka kwa wazazi wao.

Naibu Waziri huyo amesema kuwa siyo kwamba serikali imeshindwa kuwatengea vituo maalum watoto hao kwa ajili ya makuzi lakini kitaalam ni muhimu kwa mzazi kuwa karibu na mwanaye katika wakati huo ili kumjengea mazingira bora katika ukuaji.