Alhamisi , 15th Oct , 2020

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, imetoa tahadhari na kuagiza kuchukuliwa hatua za kuepuka kutokea kwa magonjwa ya mlipuko, kufuatia mvua zinazoendelea katika baadhi ya maeneo na kusababisha mafuriko na uharibifu wa miundombinu hasa kwa mkoa wa Dar es Salaam.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi.

Tahadhari hiyo imetolewa leo Oktoba, 15, 2020, jijini Dodoma na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi,  na kusema kuwa mvua hizo zina uwezekano mkubwa wa kuibuka kwa magonjwa ya kuhara damu, kipindupindu na yale magonjwa yanayoenezwa na mbu yakiwamo ya malaria na dengue.

Aidha Prof. Makubi ameagiza kuwa wananchi wanapaswa kuzingatia kanuni za afya ikiwemo, kuchemsha maji ya kunywa, kuepuka kula chakula kilichopoa, kutotapisha vyoo na kutiririsha maji machafu kutumia vyandarua pamoja na kusimamia mifumo ya maji safi, taka na mitaro.

Katika hatua nyingine Prof. Makubi ameagiza waganga wakuu wa mikoa na wilaya, kushirikiana na viongozi wengine ili kuhakikisha kila eneo lililopo chini yao haligeuki kuwa chanzo cha magonjwa ya mlipuko.