Jumatano , 15th Oct , 2014

Rais wa Tanzania Dkt Jakaya Kikwete amesema serikali itaendelea na mapambano dhidi ya matumizi na biashara haramu ya dawa za kulevya nchini ili kukabiliana na wingi la vijana kuendelea kutumia dawa hizo.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete.

Rais Kikwete ametoa kauli hiyo hapo jana mkoani Tabora wakati akihutubia taifa katika sherehe za kilele cha mbio za Mwenge zilizoambatana na kumbukumbu ya miaka 15 ya kifo cha Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Dkt. Kikwete amesema serikali imefanya jitihada mbalimbali za kukabiliana na uingizwaji wa dawa hizo hali iliyosaidia kuwakata wasafirishaji wanaotumia njia mbalimbali kusafirisha dawa hizo.

Wakati huo huo, Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesifu mbio za Mwenge wa Uhuru kuwa umekuwa moja ya chachu ya kuwaletea maendeleo ya kiuchumi idadi kubwa ya Watanzania.

Akizungumza katika maadhimisho hayo ambayo kitaifa yamefanyika mkoani Tabora, Rais Kikwete amesema jumla ya miradi ya maendeleo 1451 yenye thamani ya fedha za Tanzania shilingi bilioni 361.3 imezinduliwa na kuwekewa jiwe la msingi wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru.