Jumatano , 9th Dec , 2015

Maandalizi ya uchaguzi wa kumpata mbunge wa jimbo la Arusha mjini utakaofanyika Jumapili ijayo yamekamilika huku serikali ya mkoa huo ikiwataka wananchi kujitokeza kushiriki zoezi hilo kwa kufuata taratibu zilizopangwa.

Mkurugenzi wa jiji la Arusha Juma Idd

Akizungumza ofisini kwake mkurugenzi wa jiji la Arusha Juma Idd amesema mpaka sasa kampeni zinaendelea kwa utulivu jimboni humo na maandalizi tayari yamekamilka na anawataka wanaohusika na mchakato wa uchaguzi wakiwemo wananchi wenyewe kufuata taratibu na maelekezo ya uchaguzi ili kukamilisha zoezi hilo.

Aidha mkurugenzi amewataka wakazi wa jiji la Arusha pamoja na wadau wote wa uchaguzi kuhakikisha wanadumisha amani wakati wa uchaguzi na yeye akiwa kama msimamizi wa uchaguzi atasimamia haki katika uchaguzi na wakati wa utangazaji wa matokeo.

Awali mchakato wa kumpata mbunge jimboni hapo ulisimamishwa kutokana na kufariki kwa aliyekuwa mgombea wa nafasi hiyo kupitia chama cha ACT Wazalendo, ambapo wananchi wanategemea kupiga kura katika vituo mia saba ishirini na moja vilivyopo katika kata ishirini na tano, ambapo vyama vitano vimesimamisha wagombea katika kinyang’anyilo hicho.