Jumatatu , 25th Feb , 2019

Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, ametoa onyo kwa wadhamini wa mtuhumiwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu kufika mahakamani kila kesi inapotajwa, baada ya kukataa ombi la Wakili wa upande wa Jamhuri la kutoa hati ya kumkamata kiongozi huyo.

Kutoka kushoto, Jabir Idrissa, Mhariri wa Mawio, Simon Mkina, Mhariri na Mmiliki wa gazeti la Mawio na Tundu Lissu walipokuwa mahakamani.

 Upande wa mashtaka ukiongozwa na Wakili Simon Wankyo, alidai kuwa Lissu yuko nje ya nchi siyo kwa matibabu, bali kwa ajili ya kufanya kazi za kisiasa na kufikia hatua ya kuiomba mahakama hiyo itoe hati ya kumkamata Lissu.

"Kama itakupendeza mheshimiwa hakimu tunaiomba mahakama yako itoe hati ya kumkamata mshtakiwa kwa kuwa tunamuona anazunguka nchi mbalimbali kufanya mihadhara," amedai Simon.

Baada ya Wankyo kueleza hayo, Hakimu Simba amesema hati ya kumkamata mshtakiwa kwa sasa haiwezi kutolewa na mahakama hiyo.

"Hati ya kumkamata mshtakiwa kwa sasa haiwezi kutolewa, hivyo nawaonya wadhamini kufika mahakamani kila kesi hii inapotajwa", amesema Hakimu Simba.

Lissu kwa sasa yuko nje ya nchi kwa muda mrefu kwa ajili ya matibabu baada ya kutoka hospitali ya jijini Nairobi, Kenya ambako alikimbizwa baada ya kupata matibabu ya dharura Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma baada ya kushambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana

Lissu na wenzake wanatuhumiwa katika kesi hiyo yenye Na. 208 ya mwaka 2016, kutoa chapisho la uchochezi katika Gazeti la MAWIO, toleo Na. 182 la tarehe 14-20 Januari 2016.