Alhamisi , 27th Aug , 2015

Wananchi wametakiwa kuwa na utulivu na kutoshusha bendera za vyama wanavyo vichukia ili kuepusha migongano na vurugu wakati wa kipindi hiki cha uchaguzi.

Bendera za vyama vitatu CUF, CHADEMA na CCM

Hayo yamebainishwa na mwenyekiti wa Kijiji cha Ihanga, Christopha Ng’olo, wakati wa Uzinduzi wa kampeni za Chama cha ACT Wazalendo, ambacho kimemsimamisha Elimian Msigwa kugombea jimbo la Njombe Kusini, alisema kuwa wananchi wanatakiwa kuwa watulivu wakati huu wa uchaguzi.

Katika uzinduzi huo ambao jeshi la polisi halikuwapo ili kuimalisha ulinzi inadaiwa kuwa kabla ya kufanyika kwa mkutano kulikuwepo kwa hatihati ya kufanyika vurugu kutokana na baadhi ya wananchi kutaka kushusha bendera za Chadema ambazo zimetawala kila kona za kijiji hicho.

Ng’olo amesema kuwa wananchi hawapaswi kushusha bendera za chama chochote bila ya makubaliano na wanachama wa chama husika kwa kuwa kwa kufanya hivyo wanaweza kusababisha vurugu.

Aidha kwa upande wake afisa mtendaji wa kijiji na kaimu afisa mtendaji wa kata hiyo Aderehad Mlowe amesema kuwa juzi majira ya mchana kulitaka kutokea vurugu baada ya wananchama wa chama Cha ACT Wazarendo kutaka kushusha bendera za chama cha CHADEMA.

Amesema kuwa alitoa elimu kwa wanachama ili wasifanye hivyo bila ruhusa ya wenyechama husika.

Naye mgombea hiyo ambaye alikuwa ni mtiania wa CHADEMA Emilian Msigwa na kugombea ACT, amesema kuwa ACT haina ubaya na chama chochote cha siasa na kuwa wananchi wanatakiwa kuangalia ni nani anawafaa ili kumchagua.