Jumatatu , 2nd Mei , 2016

Idadi ya Watanzania wanaotumia huduma za kifedha zinazotolewa na mabenki nchini imekuwa hairidhishi kutokana na sababu mbali mbali mojawapo ikiwa ni kukosekana kwa hamasa juu ya matumizi ya huduma hizo.

Katika kutambua hali hiyo, Benki ya Amana yenye makao yake makuu jijini Dar es Salaam imeamua kutoa zawadi kwa Watanzania watakaoweka fedha zao katika benki hiyo kwa kipindi cha miezi mitatu mfululizo pasipo kuzichukua kama njia ya kuwafanya wajenge tabia ya kujiwekea akiba.

Meneja Masoko wa Benki hiyo Bw. Dassu Mussa, amesema hayo leo wakati wa kuanza kwa kampeni maalumu inayojulikana kama Faidika na Amana Benki ambapo katika kila baada ya miezi mitatu, benki hiyo itakuwa ikiwapatia wateja wake zawadi mbali mbali vikiwemo vifaa vya nyumbani kama vile Jokofu, Runinga, Feni na nyinginezo kulingana na kiasi halisi cha akiba ambacho mteja huyo amejiwekea kwenye akaunti yake.

Kwa upande wake, Meneja Huduma kwa Wateja wa benki hiyo Bw. Juma Msabaha, amesema kampeni hiyo itahusisha pia wateja wapya wanaojiunga na kuweka akiba zao katika benki hiyo huku ikihusisha huduma yake ya kuweka pesa kwa njia ya mtandao.