Jumamosi , 6th Jan , 2018

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa amebaini Kasoro nyingi kwenye Vyama Vikuu vya Ushirika vya Mbinga (MBICU na MBIFACU) na kuagiza uchunguzi ufanyike kuanzia jana.

Majaliwa ametoa agizo hilo jana jioni  wakati akihutubia maelfu ya wakazi wa mji wa Mbinga, kwenye viwanja vya CCM, mjini Mbinga. Waziri Mkuu amesema timu ya uchunguzi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu itakiangalia chama hicho na kukifumua chote.

Kwa upande mwingine Waziri Mkuu amewaamuru  viongozi wote wa zamani na wa sasa waripoti kwa Mkuu wa Wilaya huku  OCD akihakikisha ofisi za vyama hivyo hazifunguliwi hadi kazi ya uchunguzi itakapoanza, ili wasije kubadilisha nyaraka kwenye ofisi zao.

Aidha Waziri Mkuu ameongeza kuwa wote watakaobainika kuhusika kwenye kasoro hizo watachukuliwa hatua za kinidhamu.

Waziri Mkuu pia ameeleza kuwa Serikali imeamua kuboresha ufanisi katika mazao matano ya biashara ambayo ni Pamba, Kahawa, Chai, Korosho na Tumbaku kwa sababu yanaliingizia Taifa fedha za kigeni.