Jumanne , 13th Nov , 2018

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Afrika Kusini, Malusi Gigaba amejiuzulu nafasi yake hiyo leo Jumanne Novemba 13, 2018, kufuatia kuandamwa na tuhuma za kudanganya serikali na Umma wa watu wa Afrika Kusini.

Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani wa Afrika Kusini Malusi Gigaba.

Rais Cyril Ramaphosa amethibitisha kupokea barua ya kujiuzulu ya Gigaba leo Jumanne, ikiwa ni siku moja kabla ya Rais kukutana na washauri wake, mkutano ambao unatajwa ulipanga kumchukulia hatua kiongozi huyo.

Gigaba amekuwa chini ya shinikizo la kuachia nafasi yake kutoka kwa wanasiasa wa upinzani akidaiwa kukiuka katiba kama kiongozi kwa kudanganya juu ya masuala mbalimbali ya ndani ya nchi.

Gigaba, ambaye alikuwa waziri wa fedha kati ya Machi 2017 na Februari 2018, amekuwa kwenye wakati mgumu baada ya mwezi uliopita kulazimika kuomba msamaha kutokanana na video yake binafsi ya ngono kuvuja mitandaoni.