Jumamosi , 3rd Sep , 2022

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, ameiagiza Wizara ya Afya kufanya thathimini ya hali ya mambukizi ya UVIKO – 19 na kutoa ripoti kwa wananchi waendelee na uvaaji wa barakoa au wapumzike.

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan

Rais Samia ameyasema hayo wakati akihutubia katika kilele cha Tamasha  la Kizimkazi, lililofanyika Mkoa wa Kusini Unguja na kuhudhuriwa na viongozi wa serikali na taasisi kutoka sekta binafsi, ambapo ameendelea kusisitiza watu ambao bado hawajapata chanjo ya Corona kuhakikisha wanachanja.

“Niwaombe sana Wizara ya Afya waangalie hali ilivyo, hali inaonesha watu wamechoka barakoa, wafanye tathimini watuambie tuendelee kuwa nazo au tupumzike”- Amesema Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan

Aidha Rais Samia ameeleza kuwa tayari serikali itaendelea kuweka nguvu kubwa kwenye elimu ya Tanzania hasa katika masomo ya sayansi, kwa ujenzi wa miondombinu na kuongeza idadi ya walimu wa masomo hayo, ili kuwawezesha wanafunzi kupata elimu bora.

“Suala la elimu huku Kusini Unguja bado hatupo vizuri, tutajitahizi kuzipunguza changamoto hizo ikiwa pamoja na kuongeza idadi ya walimu wa masomo ya sayansi” – Amesema Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan