Jumapili , 20th Mar , 2016

Wananchi wa Zanzibar leo wamejitokeza kwa uchache kushiriki kupiga kura katika uchaguzi wa marudio uliomalizika kwa amani huku ukishuhudia ulinzi mkali katika kila maeneo ya visiwa vya Unguja na Pemba.

Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein akipiga kura katika kituo cha Skuli ya Msingi ya Bungi.

Uchaguzi huo wa marudio umefanyika kumchagua rais, wajumbe wa baraza la wawakilishi na madiwani, baada ya kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi Oktoba 28, mwaka jana na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar Bw. Jecha Salim Jecha kwa madai ya uchaguzi kuvurugika.

Rais wa Zanzbar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein, alishiriki kupiga kura leo asubuhi katika kituo cha Shule ya Msingi Bungi na kuongea na vyombo vya habari kwa ufupi kuhusu uchaguzi huo uliosusiwa na baadhi ya vyama vya siasa.

Maeneo mengi ya biashara ya Ugunja hususani ya Darajani na Pemba Wilaya ya Wete yalionekana yakiwa yamefungwa wakati zoezi la upigaji kura likiendelea, huku pia wengi wa watu waliojitokeza kupiga kura wakiwa wanawake.

Uchaguzi huo unafanyika licha ya chama kikuu cha upinzani cha Civic United Front CUF na vyama vingine kadhaa, kususia kwa madai ya kutotambua sababu zilizopelekea Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kufuta matokeo ya uchaguzi wa Oktoba mwaka jana.