Jumanne , 14th Jan , 2020

Baada ya Tausi kujifungua salama mtoto wa kike wiki iliyopita, msanii wa filamu Dorah amesema, bado hajafikiria kabisa kupata mtoto na hayupo tayari kwa sasa.

Msanii wa filamu Dorah

Akizungumza na  EATV & EA Radio Digital,  Dorah amesema yeye bado sana kuhusu suala hilo la kuwa mzazi na hawezi kukurupuka hata kama mwanaume wake ndiyo anataka iwe hivyo.

"Swali hilo linanikera sana kwamba mwenzio kashajifungua na wewe lini, kwa sababu kila mtu ana mipango na ratiba zake katika maisha yake, labda Tausi alitaka mwaka huu ajifungue lakini kwangu mimi nawajibu ni bado sana" amesema Dorah.

Aidha Dorah ameongeza kusema "Sio kuogopa majukumu tu, yaani hata huyo mtoto unayemleta duniani uwe umemtengenezea mazingira makubwa sana na usipofanya hivyo anaweza akaja halafu ukajutia, huwezi kutegemea mtu ni wewe mwenyewe kwanza,  kama mama unatakiwa  mwanao ajivunie, kama huna pesa itakuaje" ameongeza.

Pia amesema watu wategemee kumuona mama baada ya miaka kadhaa, na hata mpenzi wake bado hajazungumzia kuhusu hilo suala.