Jumatano , 1st Jul , 2020

Kundi la muziki wa HipHop Rostam ambalo linaundwa na wasanii Roma na Stamina, wamefanikisha kukusanya kiasi cha Shilingi Milioni 3.4 kupitia 'challenge yao ya kaka tuchati' na kununua mashine mbili za Oxygen 2 pamoja na Mashuka 68, ambayo yatasambazwa kwenye Hospitali mbili.

Kundi la Rostam Roma Mkatoliki upande wa kushoto na Stamina upande wa kulia

Zoezi hilo limetokana na challenge ya wimbo wao wa kaka tuchati, ambapo walitoa fursa ya watu kuchangia walichonacho ili kupatikana kwa vifaa vya kuwasaidia wagonjwa mahospitalini na wameulekeza msaada huo katika moja ya Hospitali iliyopo mkoani Tanga na Morogoro.

Kupitia kurasa zao za mtandao wa Instagram wameandika kuwa "Tumefanikiwa kufanya malipo Bohari ya Dawa (MSD) , na kununua mashine za oxygen 2 "Oxygen Concentrator" pamoja na mashuka 68"

"Kuanzia tarehe mosi ya mwezi Julai, tutaenda kuyakabidhi kwenye Hospitali ambazo tumependekeza,  moja iwe Morogoro mahali anapotoka Stamina na nyingine iwe Tanga anapotoka Roma Mkatoliki".