Jumatano , 6th Nov , 2019

Rapa wa kike kutoka nchini Tanzania, Rosa Ree, ameomba radhi kwa watanzania baada ya kusambaa kwa video zake, zikionesha akishikwa maungo ya kifuani kwake na msanii mwenzake aitwaye Timmy Tdat.

Rosa Ree kupitia mtandao wa kijamii wa Instagram, amepost kipande cha video fupi kilichonesha akiomba radhi kwa mashabiki na watanzania kwa ujumla.

"Ningependa kuomba radhi kwa waliokwazika  na ile video iliyosambaa mtandaoni, leo hii nimefurahi kukutana na Bodi ya Filamu Tanzania na wamenielimisha mengi kuhusiana na sanaa na kanuni zake, tutaendelea kufanya kazi pamoja ili kuweza kuifikisha sanaa ya Tanzania mbali zaidi"  ameeleza Rosa Ree.

Aidha msanii huyo ameongeza kuwa, "Nimefahamu kama msanii natakiwa nipeleke  'scripts'  yangu ya video kwenye Bodi ya filamu kabla sijaiachia na pale nitaweza kupata kibali ambacho nitaweza kuiachia, naahidi kazi zangu zitakuwa zenye kiwango cha juu".

Siku ya Novemba 5, 2019, kupitia mtandao wa Instagram zilionekana video zikimuonesha Rosa Ree, anashikwa  maungo ya kifuani kwake na msanii kutokea nchini Kenya, ambaye inasemekana ni mpenzi wake aitwaye Timmy Tdat, huku maungo yake mengine ya mwili yakionekana kuwa wazi.