Jumatano , 28th Feb , 2024

Polisi nchini Afrika Kusini jana Jumanne wamesema kuwa wamewakamata watu sita wanaohusika na mauaji ya aliyekuwa Rapa maarufu Kiernan Forbes, maarufu kama AKA mnano Februari 2023.

Mwanamuziki huyo aliyefariki akiwa na umri wa miaka 35, alipigwa risasi na kuuawa yeye na rafiki yake Tebello "Tibz" Motshoane, Februari 10, mwaka jana wakati wakitembea nje ya mgahawa maarufu mjini Durban. AKA alipanga kutumbuiza katika klabu moja ya karibu usiku huo.

Kamishna wa Polisi, Nhlanhla Mkhwanazi amewafahamisha wanahabari kwamba "msimamizi, watu wawili wenye silaha, watekaji wawili, na mwingine aliyehusika na magari wakati wa tukio, wote watafikishwa mahakamani".

Inasemekana kuwa rapa huyo alikuwa akifuatwa kimya kimya tangu alipowasili katika uwanja wa ndege wa Durban hadi alipofika mgahawani.

Afrika Kusini ni miongoni mwa mataifa yenye viwango vya juu vya mauaji duniani, na mastaa kadhaa wa muziki nchini humo wameathirika na mauaji hayo.

Itakumbukwa mwaka 2007, Mwimbaji wa muziki wa Reggae Lucky Dube alipigwa risasi mara tatu wakati akimpeleka mtoto wake wa kiume katika nyumba ya jamaa yake.