Jumatano , 7th Oct , 2020

Mtaalamu wa Afya kutoka Wizara ya Afya Dkt.Jubilate Bernald, amesema kuwa ugonjwa wa kichaa cha Mbwa ni tofauti na magonjwa mengine ambapo mtu akishaanza kuonyesha dalili za ugonjwa  huo hawezi kupata tiba.

Mfano wa mtu aliyejeruhiwa na mbwa

 

Akizungumza na East Africa Radio, katika kipindi cha Supa Breakfast amewataka watu kuchukua tahadhari mapema pale wanapokuwa wameumwa na mbwa na sio kusubiri mpaka dalili zinapoanza kuonekana.

"Ugonjwa huu ni tofauti kabisa na magonjwa mengine yoyote tunayoambiwa ukiona dalili wahi kituo cha afya, kwa sababu ugonjwa huu mtu akishaanza kuonyesha dalili hakuna tiba na moja kwa moja inakuwa anasubiria kifo" alisema Dr.Jubilate

Aidha Dkt.Jubilate amesema licha ya dalili ya ugonjwa huo kufafana na magonjwa mengi ameitaja dalili pekee ya ugonjwa huo ni wagonjwa kuogopa maji.

“Dalili ya peke yake ya kumtambua mtu mwenye ugonjwa huo zaidi huwa anaogopa maji na mwanga, ukimuekea maji anaweza akaogopa au akakimbia nakumwaga yale maji,anadhoofu, anabweka kama mbwa na wanakuwa na nguvu sana, wakorofi"alisema Dkt.Jubilate

Kwa mujibu wa wataalamu wa afya Kichaa cha mbwa, ni ugonjwa ambao  unaambukizwa kwa kungatwa na mbwa mwenye kichaa na ugonjwa huu si kwa binadamu bali hata wanyama , wastani wakuonyesha dalili za ugonjwa huo ni wiki mbili hadi mwezi  inaweza ikazidi au chini ya hapo.