Jumatatu , 27th Mei , 2019

Afisa Habari wa klabu ya Yanga, Dismas Ten amekubaliana na ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania bara msimu wa 2018/19 ambao umekwenda kwa Simba, akisema kuwa ubingwa wao hauna wasiwasi.

Dismas Ten

Katika ukurasa wake wa Instagram, Dismas amesema kuwa ni wakati sasa wa klabu zingine zilizobaki kujitathmini na kujua ni wapi wamekosea ili waje upya msimu ujao.

"Ligi inamalizika kesho, yes..! bingwa amepatikana, ni bingwa 'no doubt'..!. Wengine acha tuone wapi tulikosea tujipange kwa msimu ujao..! .", amesema Dismas.

"Ndiyo soccer ilivyo, timu zote zilipambana lakini moja imeupata, hiyo ndiyo maana ya ligi..! .", ameongeza.

Kuelekea mechi za mwisho za ligi ambazo zitapigwa siku moja na muda mmoja, kesho Jumanne saa 10:00 jioni, Yanga itakuwa nyumbani ikiikaribisha Azam FC katika uwanja wa Taifa huku wapinzani wao Simba wakielekea Morogoro kuwafuata Mtibwa Sugar, ambako wnatarajia kukabidhiwa kombe lao la ligi kuu msimu huu.

Michezo mingine itakayopigwa kesho katika kukamilisha ratiba ya ligi ni pamoja na Coastal Union ambayo itawakaribisha Singida United, JKT Tanzania itakayowaalika Stand United, Mwadui FC dhidi ya Ndanda FC, Ruvu Shooting dhidi ya Alliance FC, Mbeya City watamenyana na Biashara United, Mbao FC dhidi ya Kagera Sugar, Tanzania Prisons ikiwakaribisha Lipuli FC, huku African Lyon ikicheza na KMC.