Jumanne , 21st Jun , 2016

Pamoja na mashindano ya vijana chini ya miaka 19 ya mchezo wa kriketi kwa nchi za Afrika kufanyika mwezi wa tisa mwaka huu nchini Afrika Kusini tayari timu ya kriketi ya Tanzania chini ya umri huo imeanza kambi maalumu ya mazoezi jijini Dar es Salaam

Wachezaji wa timu ya Kriketi ya Tanzania chini ya miaka 19.

Kikosi cha wachezaji 25 wa mchezo wa criket wa chini ya miaka 19 wa Tanzania pamoja na kocha wao Kharil Rhemtulah wameingia kambini kwaajili ya mazoezi ya awali kabla ya kuanza mazoezi ya mwisho hapo baadae kujiandaa na michuano ya Afrika itakayofanyika mwezi wa tisa nchini Afrika kusini.

Akizungumzia kambi hiyo maalumu ambayo itafanyika kwa mzunguko katika mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Mwanza na Arusha kocha Rhemtulah amesema pia kutafanyika kliniki maalumu kwa walimu na wakufunzi kutoka kamati ya ufundi ya chama cha kriketi nchini TCA kwakushirikiana na makocha kutoa mafunzo ya mchezo huo katika maeneo hayo.

Aidha Kharil amesema katika mizunguko ya kambi hiyo maalumu watatumia fursa hiyo kung'amua vipaji vipya katika mchezo huo hasa kwa vijana nakuwajumuisha katika programu ya timu za taifa kwaajili ya mashindano mbalimbali ya kimataifa msimu ujao.

Akimalizia Kharil ambaye pia ni mchezaji wa timu ya wakubwa wa mchezo huo nchini amewataka Watanzania kuisaidia timu hiyo kwa uiwezesha kwa vifaa vya mchezo wenyewe kwaajili ya mazoezi na mechi lakini pia akatoa wito kwa Serikali kuwatafutia maeneo maalumu vijana katika mikoa na wilaya zao ili waweze kucheza mchezo huo katika maeneo mengi nchini kama ilivyo kwa michezo mingine kama soka, kikapu na mpira wa pete[ netiball] na mingineyo.