Jumanne , 21st Jan , 2020

Klabu ya Aston Villa imethibitisha kumsajili mshambuliaji Mbwana Samatta kwa mkataba wa miaka minne na nusu kuitumikia klabu hiyo hadi mwezi Juni, 2024.

Mbwana Samatta

Usajili huo umekamilishwa kwa ada ya Pauni milioni 8.5 na moja kwa moja ataingia katika kikosi kinachojiandaa na mchezo wa ligi leo Jumanne, Januari 21 dhidi ya Watford japokuwa kuna uwezekano mdogo wa kuanza kwenye kikosi cha kwanza.

"Kwangu mimi ina maana kubwa sana, nchini Tanzania watu wanapenda soka na wanapenda kuangalia Premier League. Itakuwa ni kipindi ambacho Watanzania wanakwenda kumuangalia mchezaji wao akiichezea Aston Villa", amesema Samatta katika mahojiano yake ya kwanza na mtandao wa klabu hiyo.

Kuelekea kwenye kampeni ya ligi na michuano mingine, Samatta atakuwa na kibarua kuanzia wikiendi hii ambapo katika mechi 10 za kwanza, Aston Villa itacheza na Watford (H), Leicester City (H), Bournemouth (A), Tottenham Hotspurs (H), Southampton (A), Sheffield United (H), Chelsea (H), Newcastle United (A), Wolverhampton (A), Liverpool (A).

Aston Villa inakamata nafasi ya 18 katika msimamo wa ligi kuu nchini Uingereza, ikiwa imeshinda mechi sita, imefungwa mechi 13 na sare nne.