Jumapili , 19th Jan , 2020

Kocha wa klabu ya Yanga, Luc Eymael ameonesha kutofurahishwa na waamuzi wa mchezo wa ligi dhidi ya Azam FC uliopelekea kufungwa bao 1-0 jana Jumapili, Januari 19

Kocha wa Yanga na wachezaji

Mchezo huo uliopigwa katika Uwanja wa Taifa, umeshuhudia Yanga ikipoteza mchezo wa pili mfululizo chini ya kocha huyo katika ligi kuu.

Akizungumza baada ya kumalizika kwa mchezo huo, Eymael amesema kitendo akichofanyiwa na mwamuzi wa kati cha kukataa kumpa mkono amekitafsiri kama ni ubaguzi dhidi yake.

"Nataka nizungumze suala la waamuzi, kweli ile ni kadi nyekundu lakini kabla mchezaji wa azam hajafanyiwa madhambi alimvamia mchezaji wa Yanga, mwamuzi wa pembeni alikuwepo pale lakini akasema hakuona kitu. Mwambuzi akaja kwangu kunipa kadi ya njano nikampa mkono lakini akaukataa, kwanini mko hapa, ni kwasababu mimi ni mzungu?, ni ubaguzi dhidi ya watu weupe?, kiukweli nimefadhaika sana", amesema Luc

"Kwa hali hii ilivyo, ninafikiria juu ya hatma yangu hapa, nitaongea na kamati juu ya hatma yangu. Siridhishwi na kinachoendelea hapa, sizungumzii juu ya Azam FC bali nazungumzia juu ya vitu hivi vingine kwenye mchezo", ameongeza.

Kuhusiana na mchezo kiufundi, kocha Eymael amesema kuwa bahati haikuwa upande wao katika mchezo huo, kwani walicheza vizuri kipindi cha kwanza na kutengeneza nafasi za kutosha lakini hazikuzaa matunda na mwisho wakafungwa bao ambalo amesema hakuelewa limetokeaje.

Kocha huyo sasa amepoteza mechi ya pili mfululizo katika ligi, akifungwa jumla ya magoli manne, huku timu yake ikiwa haijafunga bao lolote.