Ijumaa , 17th Feb , 2017

Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger amesema kuwa ataendelea kufundisha soka kwa msimu ujao, kwenye klabu hiyo hiyo, au mahala pengine.

Arsene Wenger - Kocha wa Arsenal

 

Wenger, mwenye umri wa miaka 67, amekuwa na wiki ya aibu baada ya timu yake kuchapwa mabao 5-1 na Bayern Munich, siku ya Jumatano, kwenye mchezo wa hatua ya 16 bora ligi ya mabingwa Barani Ulaya.

Baada ya kipigo hicho, baadhi ya wachezaji wa zamani wa klabu hiyo, wamesema mwisho wa Mfaransa huyo, kufundisha The Gunners, umewadia.

Lakini Wenger amesema kukosolewa amezoea na anafanya kile anachokiamini, ila kila kitu kitajulikana Machi au Aprili mwaka huu, kama ataondoka au kubaki kwenye klabu hiyo ya London.

"Haijarishi kinachotokea nitaendelea kufundisha msimu ujao. ama hapa Arsenal au sehemu nyingine, nina uhakika na hilo". Alisema Wenger.