Alhamisi , 30th Jun , 2016

Ryan Giggs anajiandaa kuhitimisha miaka 29 ndani ya klabu ya Manchester United aliyojiunga nayo tangu akiwa kinda baadaye mchezaji wa kutegemewa na akamalizia mpira wake akiwa kama kocha msaidizi kwa makocha wa awamu mbili tofauti.

Kocha msaidizi ya Manchester United Ryan Giggs.

Kutokana na kuona uwezekano wa kuwa kocha mkuu wa United umefutika rasmi baada ya klabu hiyo kumpa nafasi hiyo Jose Mourinho aliyekuwa kocha msaidizi wa timu hiyo kwa awamu tofauti Ryan Giggs sasa ni rasmi hatoendelea na kibarua katika benchi la ufundi la timu hiyo.

Raia huyo wa Wales amekataa ofa ya kuwa katika benchi dogo la ufundi la timu ya Manchester United chini ya kocha mpya wa timu hiyo Mreno Jose Mourinho, akiamini kama United ingempa yeye nafasi hiyo ya juu kama walivyokubaliana baada ya kuhudumu kama kocha msaidizi wa timu huyo chini ya makocha waliopita David Moyes na Louis van Gaal.

Wawakilishi wa Giggs hivi sasa wako katika makubaliano na United juu ya malipo ya kuvunja mkataba wake wa mwaka mmoja uliobaki.

Kiungo huyo mshambuliaji wa zamani wa United mwenye miaka 42 anataraji kuanza uchambuzi kwa siku 10 katika runinga ya ITV wakifanya uchambuzi wa michezo ya michuano ya Euro 2016 kuanzia hii leo wakati wa hatua ya robo fainali.

Giggs ametengeneza rekodi katika klabu hiyo akiichezea michezo 963 baada ya kujiunga akiwa kinda wa miaka 14 mnamo mwaka 1987, na alifanikiwa kushinda mara mbili ubingwa wa ligi ya mabingwa barani Ulaya, huku pia akishinda ubingwa wa ligi kuu ya England EPL mara 13 na pia kutwaa taji la michuano ya kombe la FA mara nne [4].