Ijumaa , 21st Dec , 2018

Shirikisho la soka nchini (TFF), limeweka wazi kuwa linakuja na mpango wa kutengeneza mkakati wa kusaidia vipaji vya vijana wa Serengeti Boys viweze kuendelezwa kupitia kuvibana vilabu vya ligi kuu viweze kuwapatia nafasi.

Rais wa TFF Wallace Karia

Hilo limebainishwa na Rais wa Shirikisho hilo, Wallace Karia alipokuwa akieleza mpango endelevu wa timu hiyo kwaajili ya faida za timu ya taifa ya wakubwa (Taifa Stars), ambapo amesema wataweka kanunu za kuhakikisha vilabu vinawapa nafasi vijana.

''Tunataka tupitishe Kanuni ya kuwalinda Vijana katika timu mbalimbali, wasipopata nafasi ya kucheza wapate nafasi ya kupelekwa kwa mkopo sehemu nyingine ili kupata muda mwingi wa kucheza'', amesema.

Katika kuboresha zaidi kikosi cha Serengeti Boys ambacho kitashiriki, michuano ya AFCON kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17, TFF, imeongeza nguvu kwenye benchi la ufundi kwa kumleta kocha wa zamani wa Hull City Andy Marc Reagan kuwa kocha mkuu.

Serengeti Boys imekuwa na mwendelezo mzuri wa matokeo ambapo, April mwaka huu ilitwaa ubingwa wa CECAFA kabla ya Jumapili Desemba 16, kutwaa ubingwa COSAFA.