Jumanne , 31st Jan , 2023

Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul amesema kuwa, miongoni mwa mipango ya Serikali katika kuziendeleza timu za Watoto ni pamoja na kuendelea kuratibu mashindano ya michezo ya Shule za Msingi (UMITASHUMTA) na Shule za Sekondari (UMISSETA).

Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Pauline Gekul

Mhe. Gekul amesema hayo Januari 31, 2023 Bungeni Dodoma, wakati akijibu swali la Mhe. Husna Sekiboko wa Viti Maalum, aliyeuliza Ni upi Mkakati wa Serikali katika kuziendeleza timu za michezo za Watoto.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Gekul ameeleza kuwa, Mkakati wa Serikali ni pamoja na kukarabati miundombinu ya michezo katika shule 56 teule za michezo pamoja na usajili wa vituo vya michezo vya watoto.

" Serikali inaendelea kuhamasisha wadau mbalimbali kuandaa mashindano ya timu za watoto na kuwajengea mazingirawezeshi ya kuanzisha na kuendeleza vituo vya michezo kwa watoto" amesisitiza Mhe.Gekul.

Akijibu swali la Nyongezala Mhe. Sekiboko kuhusu lini ujenzi wa shule teule56 za michezo ikiwemo ngapi katika Mkoa wa Tanga utaanza,Naibu Waziri Gekul amesema kuwa tayari kiasi cha Shilingi takriban Bilioni 2 kimeanza kutumika katika ujenzi wa shule hizo kwenye mikoa mbalimbali nchini, ikiwemo Mkoa wa Tanga ambao Shule ya Tanga School na Nyerere Memorial ndio zilizochaguliwa.