Alhamisi , 26th Mei , 2016

Kikosi cha timu ya soka ya Taifa ya Tanzania – Taifa Stars, chini ya makocha Boniface Mkwasa na Hemed Morocco kinatarajiwa kuondoka kesho saa 12.00 alfajiri kwenda Nairobi, Kenya kucheza na Harambee Stars katika mchezo wa kirafiki wa kimataifa.

Kikosi cha timu ya soka yaTaifa ya Tanzania [Taifa Stars].

Mchezo huo ni maandalizi ya kujiandaa kucheza mchezo muhimu kabisa dhidi ya Mafarao wa Misri Juni 4, mwaka huu katika mchezo wa kuwania kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON-2017) wakati Kenya pia itakuwa na mchezo dhidi ya Congo.

Mkwasa maarufu kama Master, alitangaza kikosi cha timu hiyo Mei 18, mwaka huu mbele ya waandishi wa habari kwenye Ukumbi wa mikutano wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Ilala jijini Dar es Salaam.

Mchezo huo unadumisha uhusiano na upendo wa enzi wa nchi za Kenya na Tanzania na umeingizwa kwenye orodha ya viwango vya Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA) hivyo ni wazi utakuwa na ushindani wa kutosha.

Timu hiyo inaondoka ikiwa na kikosi kamili huku ikikosa huduma ya nahodha na mshambuliaji wake wa Kimataifa anayecheza nje ya nchi Mbwana Ally Samatta ambaye siku hiyo ya Juni 4 atakuwa na majukumu na timu yake ya Genk ya Ubelgiji wakati ikipigania kusaka tiketi ya kucheza michuano ya vilabu barani Ulaya.

Kikosi kamili cha Stars kina makipa, Deogratius Munishi (Young Africans), Aishi Manula (Azam FC) na Benny Kakolanya (Tanzania Prisons).

Mabeki ni Mwinyi Haji na Juma Abdul (Young Africans), Aggrey Moris, David Mwantika na Erasto Nyoni (Azam FC), Mohammed Hussein (Simba) na Vicent Andrew (Mtibwa Sugar).

Viungo ni Himid Mao, Farid Mussa (Azam), Jonas Mkude na Mwinyi Kazimoto (Simba), Mohammed Ibrahim na Shiza Kichuya (Mtibwa Sugar), Ismail Issa (JKT Ruvu), Juma Mahadhi (Coastal Union) na Hassan Kabunda (Mwadui FC)

Washambuliaji ni Thomas Ulimwengu (TP Mazembe), Mbwana Samatta (KDC Genk), Elias Maguli (Stand United), Ibrahim Ajib (Simba), John Bocco (Azam), Deus Kaseke (Young Africans) na Jeremiah Juma (Tanzania Prisons).