Alhamisi , 16th Jan , 2020

Kwa mujibu wa ripoti ya mtandao wa Dail Mail nchini Uingereza, Shirikisho la Soka barani Ulaya UEFA limebadili mfumo wa kikosi cha mwaka kilichopigiwa kura na mashabiki kwa kumtoa Ng'olo Kante na kumuweka Cristiano Ronaldo.

Kikosi bora cha UEFA mwaka 2019, Ng'olo Kante na Cristian Ronaldo

Kikosi hicho kilichopigiwa kura na mashabiki dunia nzima kilitangazwa Jumatano, Januari 15, 2020 kikiwa na mfumo wa 4-2-4, ambapo wachezaji waliotajwa katika kikosi hicho ni Golikipa: Alisson, Walinzi: Trent Alexander-Arnold, Matthijs De Ligt, Virgil Van Dijk na Andy Robertson, Viungo: Frenkie De Jong na Kevin De Bruyne pamoja na Washambuliaji: Lionel Messi, Robert Lewandowski, Cristiano Ronaldo na Sadio Mane.

Inaelezwa kuwa Ronaldo alipata kura chache dhidi ya washambuliaji wenzake, Messi, Lewandowski na Mane na wakuu wa shirikisho hilo hawakuridhishwa na Ronaldo kuachwa kwake, hivyo wakaamua kufanya mabadiliko hayo na kupelekea sintofahamu kubwa.

Inadaiwa kuwa kikosi hicho kilikuwa tayari kutangazwa tangu wiki iliyopita lakini suala la Ronaldo ndilo lililopelekea kucheleweshwa kwa taarifa hiyo kutangazwa

Lakini msemaji wa UEFA akijibu kuhusu mabadiliko hayo amesema, "mabadiliko hayo ya kumtoa Kante na kumuweka Ronaldo yamefanywa kwa kuzingatia mafanikio yake katika michuano ya 'Nations League' na mfumo wa kikosi cha mwaka huu umefanywa ili kuendana na kura zilizopigwa na mashabiki pamoja na mafanikio ya wachezaji katika michuano mbalimbali ya Ulaya".

Miaka iliyopita, mashabiki walikuwa wakichagua wachezaji pamoja na mifumo, ambapo miaka mitano kati ya sita iliyopita ulitumika mfumo wa 4-3-3 na mwaka 2017 ulitumika mfumo wa 4-4-2.