Jumatatu , 23rd Mei , 2016

Mwamuzi Israel Mujuni Nkongo wa Dar es Salaam, Jumatano Mei 25, 2016 ameteuliwa kuwa mwamuzi atakayechezesha mchezo wa fainali za Kombe la Shirikisho la TFF kati ya timu za Yanga na Azam zote za jijini Dar es Salaam mchezo utakaopigwa Jumatano hii.

Mwamuzi Israel Mujuni Nkongo wa Dar es Salaam [katikati] akiwa na mabosi wa TFF.

Mchezo huo utakaoanza saa 10.30 jioni utapigwa kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam huku waamuzi wasaidizi watakuwa Ferdinand Chancha wa Mwanza (line 1) na upande wa pili ni Soud Lila wa Dar es Salaam (line 2) na mwamuzi wa akiba ni Frank Komba wa Dar es Salaam pia na Kamishna wa mchezo huo atakuwa Juma Mgunda wa Tanga.

Nkongo amekuwa haaminiki sana na wadau wa Yanga hasa wakikumbuka mchezo wao uliopigwa miaka kadhaa iliyopita ukichezeshwa na mwamuzi hiyo ambaye baadaye alipokea kipigo kutoka kwa wachezaji wa Yanga katika mchezo ambao Azam iliibuka na ushindi wa bao 3-1 na baadhi ya wachezaji wa timu hiyo kupata adhabu kufuatia kitendo cha kumpiga mwamuzi huyo ambaye sasa wanakutana naye tena akichezesha mchezo huo dhidi ya timu ile ile ya Azam.

Kwa mujibu wa kanuni za Ligi Kuu msimu wa 2015/16, mabingwa wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara msimu wa 2015/16 wataiwakilisha nchi katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika msimu wa 2016/17 ambapo nafasi hiyo tayari imechukuliwa na Young Africans.

Kadhalika Azam ina tiketi tayari ya kushiriki Kombe la Shirikisho Barani Afrika kwa kufika fainali za ASFC ingawa kanuni zinataka bingwa ambako kwa upande wa Yanga wana tiketi ya michuano ya juu zaidi ya shirikisho. Mvuto wa mchezo wa Jumatano ni ushindani wa soka na zawadi kwa bingwa.

Fainali za Kombe la Shirikisho zinakuja baada ya mchuano ulioshindanisha timu 64 za Ligi Kuu Tanzania Bara - VPL (16); Ligi Daraja la Kwanza -FDL (24), Ligi Daraja la Pili – SDL (24).