Alhamisi , 23rd Jan , 2020

Uongozi wa klabu ya Yanga umeendelea kusisitiza kuwa unasubiri barua rasmi ya adhabu iliyotolewa na Kamati ya Uendeshaji wa Ligi kufuatia madai ya utovu wa nidhamu yaliyofanywa na wachezaji wake na kocha.

Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi, Stephen Mguto

Akiongea na EATV/Radio Digital, Afisa Habari wa Yanga, Hassan Bumbuli amesema kuwa wao hawawezi kulalamikia chochote kwa sasa bali wanasubiri barua rasmi kutoka kamati hiyo.

"Siwezi kuzungumzia hilo, sijalalamika na wala Yanga haijalalamika bali  tumesema tunasubiri taarifa tuisome na tujiridhishe na kanuni walizotumia ndio tujue tunakubali au tunakataa", amesema Bumbuli.

Jumatano, Januari 22, Kamati ya Uendeshaji wa Ligi ilitoa adhabu kwa kuwafungia mechi 3 na faini ya Sh. 500,000 wachezaji Kelvin John na Majaliwa Shaban wa Mbeya City na Mrisho Ngassa, Ramadhani Kabwili na Cleafas Sospeter wa Yanga kwa kosa la kugoma kuingia vyumba vya kubadilishia nguo, huku pia ikitoa onyo kwa kocha wa Yanga, Luc Eymael kutokana na kauli yake kwa mwamuzi.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi, Stephen Mguto ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Uendeshaji amesema kuwa kamati hiyo ya maamuzi haiitwi 'kamati ya saa 72' kama inavyoitwa na watu wengi.

"Hii sio Kamati ya saa 72 kama watu wanavyopenda kuiita, hii ni kamati ya uendeshaji wa ligi lakini kuna watu tu na utashi wao walitaka maamuzi yafanyike kwa uharaka zaidi ndio wakaita hivyo", amesema Mguto.