Ijumaa , 29th Jul , 2022

Kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa wilaya ya Hai Lengai Ole Sabaya, imeahirishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mjini Moshi, kwa kile kilichoelezwa mahakamani kwamba mshtakiwa wa kwanza Lengai Ole Sabaya, amefanyiwa upasuaji wa kichwa.

Lengai Ole Sabaya

Upande wa utetezi katika kesi hiyo inayomkabili Sabaya na wenzake umeieleza Mahakama kuwa mshtakiwa huyo, amefanyiwa upasuaji wa kichwa na anahitaji uangalizi maalum nje ya gereza

Kutokana na upasuaji huo, upande huo wa utetezi umeiomba mahakama kumuachia kwa dhamana mshtakiwa huyo hadi hapo upelelezi wa shauri hilo utakapokamilika.

Wakili Bwemelo, amesema awali upande wa Jamhuri ulipoifungua kesi hiyo, uliieleza Mahakama kuwa upelelezi umekamilika lakini katika hali isiyo ya kawaida wameendelea kudai kuwa upelelezi haujakamilika jambo ambalo linachelewesha utoaji wa haki kwa washtakiwa hao.

Awali Wakili wa Jamhuri Sabitina Mcharo, ameiomba Mahakama hiyo kuahirisha tena kesi kwa madai ya kwamba upelelezi haujakamili lakini pia bado hawajapata kibali kutoka Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali (DPP) ili kuipa hadhi Mahakama hiyo kusikiliza kesi hiyo.