Thursday , 3rd May , 2018

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, ameonyesha kushangazwa na kitendo cha baadhi ya watu wanaolaumu mfumo wa elimu nchini, huku wakishinikiza watoto kujua lugha ya Kingereza, ili waweze kufanya vizuri darasani.

Akizungumza mbele ya wanafunzi wa chuo kikuu cha Mkwawa kilichopo mkoani Iringa, Rais Magufuli amesema ingawa ni kweli elimu yetu ina changamoto, lakini kujua lugha ya Kingereza haimaanishi kuwa mtu ndiye amesoma sana, kwani kuna mataifa hayazungumzi kingereza na yanafanya vizuri.

“Ninachotaka kusema challenge kwenye elimu ipo, lakini lazima tuwe makini katika ku-'argue', tusije tukakatili elimu yetu ambayo imeanzishwa na Baba wa Taifa, mpaka tumefika hapa halafu tuanze kujidharau. Eti mtu amemaliza 'form four' halafu hajui kuandika barua ya Kingereza, kwani kusoma ni kujua Kingereza!? Warusi wanajua Kingereza!? Kwani Wachina wanajua Kingereza!? Mbona wanatengeneza silaha za kila aina!?, mimi masters yangu nimefanya kwa Kingereza, lakini hapa nazungumza Kiswahili”, amesema Rais Magufuli.

Kutokana na hilo Rais Magufuli amewataka wanafunzi hao wa chuo kikuu cha Mkwawa ambao wapo kitivo cha elimu kwenda kuwa mfano wa kuigwa kwa kuwa walimu bora.