Tuesday , 15th Aug , 2017

Rais wa Misri, Abdel Fattah El-Sisi, amemaliza ziara yake ya siku mbili nchini Tanzania katika ziara inayotajwa kuwa na mafanikio makubwa baina ya Tanzania na taifa hilo baada ya kusaini ushirikiano kwenye sekta za afya, kilimo, pamoja na viwanda.

Akiwa nchini Tanzania Rais huyo wa Misri pamoja na mwenzake Dkt John Pombe Magufuli, wamesaini makubaliano ya ushirikiano katika nyanja mbali mbali ikiwa ni pamoja na mapambano dhidi ya rushwa, ambapo taasisi zinazopambana na rushwa za Misri na Tanzania zitashirikiana katika kubadilishana ujuzi pamoja na kusimamia miradi ya pamoja itakayoendeshwa kati ya Tanzania na Misri

Rais huyo wa Misri ameondoka leo nchini ameagwa na mwenyeji wake Rais Dkt John Pombe Magufuli ambaye alikuwa ameambatana na viongozi kadhaa waandamizi wa serikali akiwemo Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa pamoja na wakuu wa vyombo vya ulinzi na Usalama.