Monday , 10th Oct , 2016

Taasisi ya Sekta Binafsi nchini (TPSF) leo imewakutanisha wadau wote muhimu kwa lengo la kujadili mkataba wa ushirikiano wa kiuchumi baina ya nchi za Ulaya na Afrika ujulikanao kwa kifupi kama EPA

Salum Shamte

Katika mkataba huo nchi za Afrika Mashariki ikiwemo Tanzania zimejipa muda hadi Januari mwakani ili zifanye maamuzi ya kusaini au kutosaini mkataba huo.

Mkurugenzi wa Sera na Utafiti wa TPSF Gili Teri amesema hayo muda mfupi baada ya kuanza kwa majadiliano hayo na kwamba msingi mkuu utajikita katika kubaini maeneo yenye maslahi ya kiuchumi kwa taifa ili waweze kuishauri vyema serikali kabla ya kufanya maamuzi.

Awali katika mahojiano na waandishi wa habari, Makamu Mwenyekiti wa TPSF, Bw. Salum Shamte, ameishukuru serikali kwa uamuzi wake wa busara wa kutosaini mapema mkataba huo na hivyo kuipa fursa sekta binafsi kujadili maudhui ya mkataba huo hasa baada ya kufanyiwa marekebisho ya pili miaka michache iliyopita.