Tuesday , 1st Nov , 2016

Kocha  Mkuu wa Mbeya City FC Kinnah Phiri amesema amejiandaa vizuri  ‘kuikabili’ Young Africans  kwenye mchezo wa Ligi Kuu ya soka Tanzania bara   uliopangwa kuchezwa kesho Jumatano kwenye Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

Kocha wa Mbeya City Kinnah Phiri (Kushoto)

 

Kocha Phiri amesema kuwa kuwa anaamini utakuwa mchezo mzuri na mgumu kwa sababu timu zote mbili zimetoka kushinda mechi zake zilizopita huku akiahidi ‘kuiduwaza’ Yanga kwa kipigo kutokana na maandalizi  mazuri aliyoyafanya kwa kikosi chake na kutupilia mbali hofu yoyote kutoka kwa timu hiyo akiamini timu zote hizi mbili zina mchezo sawa.

Wakati huo huo kiungo wa Mbeya City Fc, Ayoub Semtawa atalazimika  kusubiri kwa majuma mawili zaidi kuweza kurejea  uwanjani, kufuatia majeraha ya kuchanika nyama za paja mguu wake wa kulia kwenye mchezo  dhidi ya African Lyon  uliochezwa jijini Dar, wiki moja iliyopita.

Kwa mujibu wa daktari wa kikosi, Dkt. Selaphini Mushi, Semtawa  alichanika  vibaya nyama za paja  baada ya kugongwa na mlinzi wa Lyon wakati alipokuwa akijaribu kukontroo mpira wa juu na kulazimika kutolewa  nje kwa msaada baada  kushindwa kabisa kutembea  kufuatia tukio hilo lililotokea  kwenye dakika ya 60 ya mchezo huo.