Wednesday , 17th Feb , 2016

Mchezaji wa soka wa Urusi Dmitri Tarasov aliwafikishia ujumbe mashabiki wa Uturuki, kwa kuvua jezi yake na kubaki na fulana ya ndani yenye picha ya Rais wa Urusi Vradimir Putin na ujumbe, baada ya mchezo mjini Istanbul.

Kiungo huyo wa Lokomotiv Moscow, alivaa fulana yenye picha ya Putin akiwa kavaa kofia ya jeshi la wanamaji, yakiambatana na maneno yaliyoandikwa "Rais mkarimu sana".

Kitendo hicho cha kisiasa kinatokana na uhasama uliokuwepo baina ya Mataifa hayo tangu Uturuki iitungue ndege ya Urusi mwezi Novemba mwaka uliopita.

Klabu ya Lokomotive Moscow inaweza kupewa adhabu kwa sababu shirikisho la soka barani Ulaya UEFA hairuhusu ujumbe au maneno yoyote ya kisiasa wakati wa mchezo.

Katika kujilinda na hilo tukio,Tarasov alijitetea; "Ni rais wangu .Namheshimu na niliamua kuonyesha kama siku zote nipo naye na kumuunga mkono". Alikieleza chombo cha habari cha Urusi, R.Sport.

Kwenye mchezo huo wa kombe la Europa, Fenerbahce ya Uturuki ilishinda mabao 2-0.