Friday , 6th May , 2016

Yanga SC kesho inashuka Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kuvaana na Sagrada Esperanca ya Angola huku ikiwakosa wachezaji wake tegemeo wa kimataifa wa Zimbabwe, kiungo Thabani Scara Kamusoko na mshambuliaji Donald Dombo Ngoma.

Afisa Habari wa Yanga Jerry Muro amesema wachezaji hao wawili hao kesho watakuwa wanatumikia adhabu ya kadi za njano walizopewa mfululizo katika mechi dhidi ya Al Ahly mwezi uliopita.

Muro amesema wanataukosa mchango wao katika mechi hiyo ambayo ni ya kwanza ya mchujo wa kuwania kucheza hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika lakini kikosi hakitoathirika kwa kuwakosa kwani kocha Mholanzi Hans van der Pluijm amekwishawaandaa wachezaji wengine wa kuziba nafasi zao.

Kwa upande wake Afisa Habari wa Shirikisho la Soka nchini (TFF) Alfred Lucas amesema wanashirikiana vizuri na Yanga katika kuhakikisha mchezo huu unachezwa salama na usiku wa jana tayari walikuwa wamekwisha wapokea Sagrada Esperanca na jioni ya leo wamefanya mazoezi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na waamuzi wakipokewa alfajiri ya kuamkia leo hii huku kamishna akipokewa saa saba ya mchana wa leo.

Mchezo huo utachezeshwa na marefa kutoka nchini Ghana ambao ni Joseph Odartei Lamptey atakayepuliza filimbi akisaidiwa na washika vibendera David Laryea na Malik Alidu Salifu, wakati Kamisaa ni Asfaw Luleseged Begashaw kutoka Ethiopia.

Viingilio vya mchezo huo ni Sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, wakati viti vya bluu na kijani watu wataketi kwa Sh. 7,000, VIP B na C watu wataketi kwa Sh 20,000 na VIP na VIP A itakuwa Sh.30,000.

Mchezo wa marudiano unatarajiwa kupigwa Mei 17 mwaka huu Uwanja wa Sagrada Esperanca zamani Quintalao do Dundo Mei 17, na utachezeshwa na marefa kutoka nchini Madagascar ambao ni Hamada el Moussa Nampiandraza atakayepuliza filimbi, akisaidiwa na washika vibendera, Velomanana Ferdinand Jinoro na Jean Thierry Djaonirina.

Yanga imeangukia katika kapu la kuwania kucheza hatua ya makundi ya Shirikisho, baada ya kutolewa na Al Ahly ya Misri katika hatua ya 16 Bora ya Ligi ya Mabingwa Afrika kwa jumla ya mabao 3-2, ikilazimishwa sare ya 1-1 Dar es Salaam na kufungwa 2-1 Alexandria.