Friday , 16th Oct , 2020

Mkuu wa wilaya ya Kisarawe Jokate Mwegelo, amesema serikali kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi haitosita kutumia mbinu mbadala za ulinzi wa Mbwa na Farasi wanaopatiwa mafunzo ili kuwadhibiti wale wote watakaochochea uvunjifu wa amani ya nchi katika kuelekea uchaguzi mkuu.

Mkuu wa wilaya ya Kisarawe Jokate Mwegelo

DC Jokate amesema hayo alipotembelea kituo cha mafunzo ya Mbwa na Farasi kinachosimamiwa na jeshi la polisi ikiwa ni ziara yake ya kujionea namna wanyama hao wanavyoweza kutumika katika kukabiliana na matukio ya uhalifu.

Aidha Jokate ameongeza kuwa nia ya serikali ni kuona Taifa linakuwa na utulivu wakati wote, hivyo akaiasa jamii za wakulima na wafugaji kujiepusha na migogoro ambayo imekua ikihatarisha uvunjifu wa amani kila uchwao.