Saturday , 5th Nov , 2022

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, amewaomba viongozi wa dini nchini wakiwemo wa Jumuiya ya Kiislamu ya Istiqaama Tanzania waongeze juhudi katika kutoa mafunzo ya dini ili kupunguza au kuondoa kabisa mmomonyoko wa maadili unaoikabili jamii.

 

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa

Waziri Mkuu amesema viongozi wa dini, viongozi wa umma wana wajibu mahsusi wa kuilea jamii, kwa kutoa mafundisho sahihi na endelevu ya dini ili kuiwezesha kutambua na kufuata yote yaliyo mema kama ilivyo amrishwa na Mwenyezi Mungu na kuacha kabisa yote mabaya yanayomchukiza.

"Katika suala hili la malezi, niendelee kuwasihi viongozi wa taasisi za dini kutumia vema huduma za kiroho na ibada kujenga jamii yenye tabia njema, utii pamoja na kuheshimu mamlaka zilizopo, kwa kufanya hivyo, tutawasaidia vijana wetu kuwa raia wema, wazalendo na wenye manufaa kwa nchi yao,".

Aidha Waziri Mkuu ameongeza kuwa, "Sote tumekuwa mashuhuda wa kuongezeka kwa baadhi ya vitendo viovu kama vile wazazi kuuawa na watoto wao, wanawake kuuawa na waume zao na vijana kutowaheshimu watu wazima, uvaaji wa mavazi yasiyo na stara hususani kwa wasichana na wavulana na matumizi ya dawa ya kulevya,".