Monday , 26th Dec , 2022

Umoja wa Wanawake wa Chama cha Mapinduzi (UWT), Mkoa wa Mbeya, wamemkabidhi tuzo  ya heshima Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan  ikiwa ni hatua ya kutambua mchango wake katika kuwaletea maendeleo na amani na utulivu nchini

Aidha tuzo hiyo ni ishara ya kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan katika kuboresha miundombinu ya Afya  kwa kujenga  wodi nyingi za wazazi, utoaji wa mikopo  na vipaumbele vingine kwa ajili ya kuwasaidia wanawake nchini.

Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya na Naibu Waziri wa Maji, Mhandisi Maryprisca Mahundi, amesema tuzo hiyo iliyotolewa na Umoja wa UWT Mkoa wa Mbeta ni sehemu ya kutambua mchango wa Rais Samia Suluhu  katika kuboresha sekta ya maji ambapo kwa sasa huduma ya maji inapatikana kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na ilivyokuwa miaka ya nyuma.

“Zaidi ya Sh. Trilioni  12 zimetolewa  na Serikali kwa ajili ya kujenga na kuboresha miradi mbalimbali mkoani Mbeya Mkoa ikiwemo miradi ya maji,ujenzi wa vituo vya afya , ujenzi wa madarasa, pamoja na miundombinu ya barabara, “ amesema Mhandisi Maryprisca na kuongeza 

“Mheshimiwa mgeni rasmi  ni ukweli ulio wazi kuwa wanawake ndio wanaokwenda zaidi kwenye vituo vya afya kuliko wanaume, mama analijua hili nalo ameweza kutujengea hospitali kubwa za wilaya zote za mbeya kila mmoja imepatiwa bil 500 kwa ajili ya wodi tatu zinazojengwa”Alisema Mahundi

Akizungumza katika kongamano hilo mgeni rasmi Spika wa bunge Dk,Tulia Ackson amewataka viongozi wa UWT kuanzia ngazi ya chini kuwa na utaratibu wa kuandaa mikutano na wananchi ili kuwafahamisha mafanikio miradi inayotekelezwa sambamba na kuchukua kero zao na kuzipeleka kwa viongozi wa ngazi za juu ili kuzifanyia kazi na kuwaletea maendeleo wananchi hao.

Akipokea tuzo hiyo kwa niaba ya Rais Samia Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Juma Homera amewapongeza  wanawake wa Mkoa huo kwa kuandaa kongamano hilo la kutambua jitihada zinazofanywa na Serikali, huku akimshukuru  Rais Samia kwa ujenzi wa jengo la mama na mtoto kwa ajili ya kujifungulia  lililojengwa mkoani humo na kugharimu zaidi  bilioni 11.