Thursday , 23rd May , 2024

Askari wa Jeshi la Polisi mkoani Songwe wametakiwa kutambua kuwa kazi ya Polisi ni kazi takatifu ambayo majukumu yake yanahusiana na makatazo na amri za Mungu.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Songwe Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Agustino Senga

Kauli hiyo imetolewa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Songwe Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Agustino Senga alipofanya baraza na Maafisa, Wakaguzi na askari wa vyeo mbalimbali.

"Makatazo yaliyoandikwa kwenye vitabu vitakatifu yana mahusiano makubwa na kazi ya Polisi hasa katika amri za Mungu ambazo katika nyumba za ibada wanaziita dhambi huku kwetu ni uhalifu inatupasa kuzuia vitendo hivyo ili jamii iwe salama," amesema Kamanda Senga.

Kamanda Senga amesema watendaji wa Jeshi la Polisi ni kioo kwa jamii hivyo basi wanapaswa kuendelea kulinda taswira nzuri ya Jeshi la Polisi kwa Jamii kwa kutenda haki katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku ili jamii iendelee kukimbilia na kushirikiana nalo katika kutoa taarifa za wahalifu na uhalifu.

Naye, Afisa Mnadhimu wa Polisi Mkoa wa Songwe Kamishna Msaidizi wa Polisi ACP Gallus Hyera aliwasisitiza askari kufanya kazi kwa bidii kwa kuzingatia wimbo wa maadili na kauli mbiu ya Jeshi la Polisi ambayo inawataka kufanya kazi kwa nidhamu, haki, weledi na uadilifu.