Monday , 8th Sep , 2025

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amemtaka balozi wa Tanzania Nchini Japan Anderson Mutatembwa kusimamia utekelezaji wa sera ya mambo ya nje ikiwa ni pamoja na kudumisha diplomasia ya uchumi kwa kuhamasisha uwekezaji na upatikanaji wa masoko wa bidhaa za ndani.

Waziri Mkuu amesema hayo leo Jumatatu, Septemba 08, 2025 alipokutana na Balozi huyo ofisini kwa Waziri Mkuu Mlimwa jijini Dodoma.

“Ni jukumu lako kwenda kutangaza fursa zilizopo hapa nchini, tumia vizuri mahusiano yetu na Japan kupata wawekezaji katika maeneo mbalimbali, zipo fursa nyingi ambazo tunahitaji kuzipata hasa za kiuchumi, ukifika huko weka mpango wa kutembelea wawekezaji, yapo maeneo ambayo tunahitaji kunufaika”.

Amemtaka pia Balozi Mtatembwa kuweka mpango wa kuwaunganisha Watanzania waishio nchini japan na kuwahamasisha kushiriki katika fursa mbalimbali ya kiuchumi zilizopo nchini humo jambo ambalo litaiwezesha Tanzania kunufaika na hatua hizo sanjari na kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini ili kuongeza idadi ya watalii wanaoitembelea Tanzania.

“Tumia majukwaa mbalimbali kuhamaisha Wajapan kuja kuitembelea Tanzania, lengo letu ni kuhakikisha tunaongeza idadi ya watalii nchini” Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Majaliwa amemtaka balozi huyo kuweka mikakati zaidi ya kuitangaza lugha ya kiswahili nchini humo. “Ukiwa huko jitahidi kupanua wigo wa matumizi ya lugha ya Kiswahili“ amesema.