Jumanne , 19th Jan , 2021

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli, amesema kuwa mgodi wa madini ya Nickel uliopo Kabanga mkoani Kagera, ukianza basi utasaidia suala la upatikanaji wa ajira za watu milioni 8 ambazo ziliahidiwa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Magufuli

Kauli hiyo ameitoa hii leo Januari 19, 2021, wakati akizungumza na wananchi wa Ngara na Kahama, mara baada ya kushuhudia utiaji wa saini kati ya serikali na kampuni ya LZ Nickel LTD, zoezi ambalo limefanyika hii leo mkoani Kagera.

"Tuliahidi ajira za watu milioni 8, mgodi huu ukianza mapema mwaka huu tutakuwa na uhakika wa upatikanaji wa ajira za watu milioni 8, nataka wananchi wa Ngara ambao wamekaa na umaskini kwa muda mrefu na huku wamekalia mabilioni ya fedha, wakafaidi na kuona matunda ya madini haya", amesema Rais Magufuli

Aidha mbali na hayo Rais Magufuli pia, akatoa rai kwa wawekezaji, "Nitoe wito kwa wawekezaji wengine, Tanzania ni sehemu sahihi ya uwekezaji waje, tuna madini ya kila aina , karibu kila mkoa kuna dhahabu, mje mchimbe Uranium mkapigane kule na mabomu ya Nyuklia".