Jumapili , 4th Dec , 2022

Kijana mwenye umri wa miaka 19, mkazi wa Kafukola wilayani Kalambo, anashikiliwa na Jeshi la polisi mkoani Rukwa kwa kosa la kumuua bibi yake mwenye umri wa miaka 80 baada ya bibi huyo kumnyang'anya vitenge na fedha mpenzi wa mjukuu wake huyo.

Vitenge

Imeelezwa kuwa vitenge na fedha hizo zilikuwa ni za Bibi na kijana alichukua bila ridhaa ya Bibi yake na kwenda kumpa mpenzi wake na bibi aliporudi shamba na kutovikuta vitenge na fedha aliamua kwenda kuvichukua kwa mpenzi wa mjukuu wake na ndipo kijana akaamua kujichukulia sheria mkononi.

Akielezea kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa ACP Theopista Mallya, amesema kijana huyo alimtaka bibi yake amapatie fedha na nguo alizotumiwa na mtoto wake ili yeye kijana ampatie mpenzi wake na baada ya bibi kumkatalia akaamua kujichukulia sheria mkononi.

Aidha katika hatua nyingine Jeshi la Polisi linawashikilia watu wawili wakiwa na vipande 11 vya meno ya Tembo huku pia likimshikilia Mtendaji wa Kata ya Mpombwe wilayani Kalambo kwa tuhuma za rushwa katika harakati zake za kuwaondosha watuhumiwa waliokamatwa kwa kujihusisha na ramli chonganishi maarufu kama lambalamba.