Jumatatu , 21st Jan , 2019

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Hai aliyefahamika kwa jina la Kumotola Kumotola amejikuta akiingia mikononi mwa polisi kwa madai ya kulizuia jeshi la polisi kufanya kazi yake.

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Hai akiwa mikononi mwa polisi

Hali hiyo imemkuta Katibu huyo baada ya kuratibu maandamano ya baadhi ya wananchi ambao walifika  ofisini kwa Mkuu wa Wilaya ya Hai Lengai Ole Sabaya kwa ajili ya kuwasilisha malalamiko dhidi ya wapinzani wao wilayani humo.

Akizungumza na waandamanaji hao, Lengai Ole Sabaya amesema hakuna kiongozi yeyote atakayeruhusiwa kulizuia jeshi kufanya kazi na yeyote atakayefanya hivyo atachukuliwa hatua za kisheria.

"Tumesitisha ufanyaji wa siasa kwa vyama vyote kwa sababu uchaguzi bado haujafika na hata tulipofikia kwa sasa mtu yeyote atakayehusika kulizuia jeshi la polisi achukuliwe hatua."

"Na nyinyi CCM kama mnalalamika mtumie njia ambayo ni rasmi lakini si kufanya maandamano." ameongeza Sabaya