Ijumaa , 27th Jan , 2023

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye amesema tayari maoni ya wadau kuhusu mapendekezo ya sheria ya huduma za habari yamekabidhiwa katika ofisi  ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG)

Tayari ofisi  ya Mwanasheria Mkuu imesema imeanza mchakato wa kupitia mapendekezo hayo ya sheria ya huduma za habari 

Hatua hiyo inafanyika kabla ya Ofisi ya AG kuwasilishwa Muswada huo  bungeni ili kusomwa kwa mara ya kwanza, ya pili na hatimaye kupitishwa kuwa sheria.

“Kuhusu mchakato wa mapitio ya sheria za habari Namba 12 ya Mwaka 2016, nafurahi kuwajulisha kuwa baada ya majadiliano ya muda mrefu na wadau mbalimbali, hatimaye majadilioano yamekamilika na nyaraka za maeneo yote tuliyokubaliana kufanyia mabadiliko zimewasilishwa kwa Mwanasheria Mkuu,” amesema Waziri Nape akiwa jijini Dodoma wakati akizungumzia hatua zilizofikiwa kuhusu mchakato mabadiliko sheria ya habari.

Hata hivyo, Deodatus Balile ambaye ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) amesema, mchakato huo mpaka kufikishwa bungeni una hatua zake na kwamba, inachofanya serikali ni utaratibu wa kawaida kazisa katika kuelekea mabadiliko ya sheria hiyo.

“Mchakato bado upo kwenye mstari ule ule, mpaka sasa matumaini yetu yapo juu katika kufikia kile tunachokihitaji. Serikali bado inapitisha mapendekezo yetu katika hatua zile zile za kawaida.

“Sisi tungetamani kasi zaidi kama alivyoshauri Mheshimiwa Rais Samia (Sukuhu Hassan) kwamba, tulimalize,” alisema Balile akizungumzia leo tarehe 27 Januari 2023 kauli ya Nape kwamba, mapendekezo ya wadau wa habari yapo katika ofisi ya AG. 

Muungano wa wadau wa habari (CoRI) umefanya vikao viwili na serikali katika kuelekea mabadiliko ya sheria ya habariu.

Wadau hao nchini wanashauri marekebisho kwenye vipengele mbalimbali vya sheria hiyo ikiwa ni pamoja na kifungu cha sita (e) kinachoeleza magazeti kupatiwa leseni kila mwaka badala ya usajili wa moja kwa moja.

Pia marekebisho dhidi ya kifungu cha saba (2) (b) (iv) kinachoelekeza vyombo vya habari kutangaza au kuchapisha habari na masuala yenye umuhimu kwa Taifa kadiri itakavyoelekezwa na serikali, wadau wakielezea kuwa kipengele hiki kinaingilia uhuru wa uhariri.

Sheria nyingine zinazolalamikiwa ni pamoja na sheria ya mawasiliano ya kielektroniki na huduma za posta (EPOCA, 2010), sheria ya Makosa ya Mtandaoni (2015), sheria ya Haki ya kupata Habari (2016) na kanuni za Maudhui Mtandaoni (2018).