Jumanne , 25th Aug , 2015

Wakazi wa Arusha na wafanyabiashara mbalimbali wamelalamikia tatizo la kukosekana kwa umeme kwa muda mrefu hususani makazi hali inayoathiri shughuli za uchumi na vipato vya wananchi wengi nchini.

Mkurugenzi wa Shirika la Umeme Nchini (Tanesco) Mhandisi Felchesmi Mramba akielezea mikakati ya shirika la Tanesco kuboresha huduma za umeme nchini kote

Aidha wafanyabiashara hao wamesema kuwa kukatika kwa umeme kumezorotesha shughuli nyingi za kiuchumi kutokana na nishati hiyo kutegemewa kwa kiasi kikubwa hivyo wameziomba mamlaka husika kuhakikisha kuwa zinashughulikia tatizo hilo .

Mkazi wa Arusha Hussein Karia amesema kuwa ili taifa liweze kuendelea inahitajika nishati ya uhalkika na si ya kubahatisha hivyo ameiomba Wizara husika kuhakikisha kuna upatikanaji endelevu wa huduma hiyo.

Mjasiriamali Faraja Mkomboi amesema kuwa tangu mgao wa umeme uanze shughuli nyingi zimesimama jambo ambalo l inapelekea hali ngumu ya kiuchumi kwa wajasiriamali wengi.

Kwa upande wake Emanuel Patson amesema kuwa ni vyema serikali ikaweka utaratibu mzuri wa kutoa taarifa kwa wananchi kabla ya kukata umeme badala ya kuwepo kwa mgao usioeleweka suala linalowashangaza wananchi wengi

Kwa Takribani muda wa miezi miwili huduma ya umeme imekua ikisuasua kwa kipindi kirefu kutokana na mgao wa umeme ambao unatokana na marekebisho yanayofanyika katika gridi ya taifa ya umeme,bado haijafahamika rasmi tamati ya mgao huo.