Ijumaa , 6th Dec , 2019

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli amewataka viongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato Mkoani Geita kuanza mara moja upanuzi wa majengo ya Hospitali ya Wilaya ya Chato kwa kuwa Serikali imeshatoa shilingi Bilioni 1 kwa ajili ya ujenzi huo.

Rais Magufuli.

Mhe. Rais Magufuli ambaye hakufurahishwa na taarifa za viongozi wa halmashauri hiyo kupoteza muda mwingi wakibishana juu ya upanuzi huo licha ya fedha za ujenzi kutolewa tangu mwezi Julai 2019, ameonya kuwa Serikali haiwezi kuvumilia kuona watu wakipata shida kwa uzembe wa viongozi wachache wa Halmashauri.

Amemuagiza Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Selemani Jafo na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chato Bw. Eliud Mwaiteleke kuhakikisha ujenzi wa majengo hayo unafanyika na kwa gharama zinazostahili.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli amemtaka Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo Dkt. Ligobeth Kalisa kuhakikisha mashine ya x-ray inafanya kazi muda wote na wananchi wanapatiwa huduma kwa wakati. Amesisitiza kuwa “sio sawa kwa Hospitali ya Wilaya kukosa huduma za x-ray, eti kwa sababu ya hakuna mikanda ya kupigia picha”.

Mhe. Rais Magufuli ametoa maagizo hayo leo tarehe 06 Desemba, 2019 aliwatembelea na kuwapa pole wagonjwa waliolazwa katika Hospitali ya Wilaya ya Chato akiwemo Mzee Zephania Petro Kanoge ambaye ndiye aliyemhamasisha kuingia katika siasa mwaka 1995.